Uhusiano kati ya Afrika Kusini na Marekani umekuwa ukikumbana na changamoto mbalimbali tangu Rais Donald Trump aingie madarakani, na hali hii imeanza kuleta wasiwasi mkubwa kwa Afrika Kusini.
Tangu alipoingia madarakani Januari 20, Rais Trump alisimamisha kwa muda misaada ya kigeni kutoka Marekani. Mnamo Februari 7, alizidi kuzidisha hali hiyo kwa kueleza sera ya Afrika Kusini ya umiliki wa ardhi kama "unyanyasaji wa kibaguzi wa ardhi" na kutishia kusitisha misaada kwa nchi hiyo.
Hatua hii ilileta pengo kubwa la kifedha kwa taasisi za afya nchini Afrika Kusini, ambazo hupokea takriban dola za Marekani milioni 448.5 (takriban shilingi za Kitanzania bilioni 1,031) kila mwaka kutoka Marekani kwa ajili ya programu za afya, ikiwa ni pamoja na kupambana na Virusi vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi.
Mwishoni mwa mwezi Februari, mikutano muhimu ya mawaziri wa mambo ya nje na mawaziri wa fedha wa nchi za G20 ilifanyika Johannesburg na Cape Town. Hata hivyo, mawaziri muhimu wa Marekani, Marco Rubio na Scott Besant, hawakuhudhuria mikutano hiyo.
Zaidi ya hayo, mnamo Februari 28, Marekani ilitangaza kujiondoa kwenye ushirikiano wa "Mpango wa Mpito wa Nishati Safi" (JETP) kupitia ubalozi wake nchini Afrika Kusini. Marekani ilikuwa imehaidi kutoa ruzuku ya dola za Marekani milioni 56 na uwekezaji wa kibiashara wa dola za Marekani bilioni 1 katika mpango huo.
Hali ilizidi kuwa mbaya zaidi wakati Marekani ilipomtangaza Balozi wa Afrika Kusini nchini Marekani, Ebrahim Rasool, kuwa "mtu asiyekubalika" na kumfukuza nchini humo. Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa balozi wa Afrika Kusini kufukuzwa tangu kumalizika kwa ubaguzi wa rangi mwaka 1994.
Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, amesisitiza mara kwa mara kuwa kuboresha uhusiano na Marekani ni jambo la kipaumbele, lakini kupata suluhisho la kudumu linaonekana kuwa changamoto kubwa.
Serikali ya Afrika Kusini inasema kuwa sheria ya umiliki wa ardhi haihusu kunyakua ardhi kutoka kwa wazungu, bali inalenga ardhi iliyoachwa au inayomilikiwa kwa madhumuni ya kubahatisha, na kwamba umiliki huo lazima uwe kwa manufaa ya umma na kwa makubaliano na wamiliki.
Hivi karibuni, ujumbe kutoka Wizara ya Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano ya Afrika Kusini ulitembelea Marekani kueleza msimamo huu.
Hata hivyo, Marekani inaonekana kuwa na wasiwasi zaidi ya suala la umiliki wa ardhi.
Serikali ya Trump inaituhumu Afrika Kusini kuwa nchi inayopinga Marekani, ikitolea mfano hatua ya Afrika Kusini kuishitaki Israel katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ).
Wakati wa mkutano wa mawaziri wa mambo ya nje wa G20 mwezi Februari, Waziri Rubio alieleza kuwa sera ya umiliki wa ardhi ya Afrika Kusini, "chuki dhidi ya Marekani," na msimamo wake dhidi ya Israel ndiyo sababu za kutohudhuria kwake mkutano huo.
Licha ya hali hii, chama tawala cha Afrika Kusini, African National Congress (ANC), kinapanga kubadili jina la barabara iliyo na ubalozi mdogo wa Marekani huko Johannesburg kutoka "Sandton Drive" hadi "Leila Khaled Drive." Leila Khaled ni mwanamke Mwarabu ambaye alijulikana kwa kuteka nyara ndege mwaka 1969 na kuwa ishara ya harakati za ukombozi wa Palestina.
Balozi Rasool, aliporudi Cape Town mnamo Machi 23, alijibu shutuma za Waziri Rubio kwa kusema kuwa hotuba yake ilikuwa "uchambuzi wa hali ya kisiasa, si shambulio la kibinafsi au la kitaifa," na aliongeza kuwa atachukulia kufukuzwa kwake kama "heshima." Msimamo wake huu wa ukaidi umepata uungwaji mkono kutoka kwa baadhi ya watu nchini Afrika Kusini.
Hata Rais Ramaphosa mwenyewe alionyesha msimamo wa kupinga wakati Rais Trump alipotoa ukosoaji wake wa kwanza kuhusu sheria ya umiliki wa ardhi ya Afrika Kusini mnamo Februari 2, akisema katika hotuba yake ya kila mwaka ya taifa mnamo Februari 6, "Hatutanyanyaswa."
Inaonekana kuwa na shaka kama hatua hizi zitasaidia kuboresha uhusiano na Marekani, jambo ambalo Rais Ramaphosa amesisitiza kuwa ni kipaumbele chake.
Kuna wasiwasi kwamba ikiwa Afrika Kusini haitaweza kurekebisha uhusiano wake na Marekani, Rais Trump anaweza kukosa kuhudhuria mkutano wa kilele wa G20 utakaofanyika Johannesburg mnamo Novemba, hali ambayo itakuwa ya kipekee na isiyo ya kawaida.