Marekani imetangaza mpango wa kukabiliana na ushawishi wa China katika sekta ya ujenzi wa meli na usafirishaji kwa kuanza kutoza ada ya kuingia bandarini kwa kampuni za usafirishaji zinazotumia meli zilizojengwa China.
Ofisi ya Mwakilishi wa Biashara wa Marekani (USTR) ilisema katika tovuti yake mnamo Aprili 17 (kwa saa za Marekani) kwamba itaanza kutoza ada kwa kampuni za usafirishaji za China, kampuni zinazoendesha meli zilizojengwa China, na meli za kubeba magari zilizojengwa nje ya nchi.
Ada hizo zitaanza kutozwa hatua kwa hatua baada ya siku 180, kuanzia Oktoba 14 mwaka huu, na zitaongezeka kila mwaka.
USTR pia ilisema kuwa ili kuhimiza ujenzi wa meli za kubeba gesi asilia iliyoyeyushwa (LNG) nchini Marekani, itahitaji kwamba kiasi fulani cha LNG kinachosafirishwa kutoka Marekani kisafirishwe kwa meli za LNG zilizojengwa Marekani kuanzia miaka mitatu ijayo.
Mwakilishi wa USTR, Jamieson Greer, alisema, "Usafirishaji wa meli ni muhimu kwa usalama wa kiuchumi wa Marekani na mtiririko huru wa biashara. Hatua hii ya utawala wa Rais Donald Trump itapunguza ushawishi wa China, kukabiliana na vitisho kwa mnyororo wa usambazaji wa Marekani, na kuongeza mahitaji ya meli zilizojengwa Marekani."
USTR ilieleza kuwa imechukua hatua madhubuti "kurejesha sekta ya ujenzi wa meli ya Marekani na kukabiliana na vitendo, sera, na mazoea yasiyo ya haki ya China katika udhibiti wake wa usafirishaji, vifaa, na ujenzi wa meli."