Chatbot Mkorofi wa Elon Musk: Awatukana Marais, Serikali za Ulaya Zaja Juu

it | Thu Jul 10 2025


Chatbot Mkorofi wa Elon Musk: Awatukana Marais, Serikali za Ulaya Zaja Juu

Mfumo wa akili mnemba (AI) wa Elon Musk, unaojulikana kama Grok, umeibua mzozo mkubwa barani Ulaya baada ya kutoa majibu ya dharau na matusi dhidi ya viongozi wa kisiasa, na kusababisha serikali kadhaa kutishia kuchukua hatua za kisheria.


Tukio la hivi karibuni limetokea nchini Poland, ambapo Grok alipoulizwa kuhusu Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Donald Tusk, alitoa jibu la kushangaza. Kwa mujibu wa chombo cha habari cha TVP, Grok alimwelezea Tusk kama "msaliti aliyeiuza Poland kwa Ujerumani na Umoja wa Ulaya (EU)." Isitoshe, mfumo huo ulizusha habari za uongo ukidai kuwa Tusk anataka kura zihesabiwe upya baada ya kushindwa katika uchaguzi wa rais wa mwaka 2025. Viongozi wengine wa Poland pia walilengwa na matamshi ya dharau.


Kufuatia tukio hilo, Waziri wa Masuala ya Kidijitali wa Poland, Krzysztof Gąfkowski, alieleza kuwa nchi yake itawasilisha malalamiko rasmi kwa Umoja wa Ulaya, akitaka uchunguzi ufanyike na kampuni ya xAI, inayomiliki Grok, ipigwe faini. "Uhuru wa kujieleza ni haki ya binadamu, si ya akili mnemba," alisema waziri huyo.


Mzozo kama huo uliibuka pia nchini Uturuki. Mahakama nchini humo imeamuru kuzuiwa kwa baadhi ya maudhui ya Grok baada ya kubainika kuwa mfumo huo ulitoa majibu ya kumvunjia heshima Rais Recep Tayyip Erdoğan na mwanzilishi wa taifa hilo, Mustafa Kemal Atatürk. Waendesha mashtaka katika mji mkuu, Ankara, wameanzisha uchunguzi wa jinai, wakisema matusi dhidi ya viongozi wa nchi ni kosa linaloweza kupelekea kifungo cha hadi miaka minne jela.


Kampuni ya xAI, inayomilikiwa na Elon Musk, ilijaribu kutuliza hali kupitia mtandao wa X (zamani Twitter), ikisema inafanya jitihada kuondoa maudhui yasiyofaa. "Tunaifunza Grok kutafuta ukweli pekee. Shukrani kwa mamilioni ya watumiaji wa X, tunabaini haraka maeneo ya kuboresha," ilieleza taarifa ya kampuni.


Wakati akizindua Grok, Elon Musk aliutambulisha kama mfumo wa AI unaotafuta ukweli kwa kiwango cha juu kabisa, hata kama ukweli huo utapingana na mitazamo inayokubalika na wengi (political correctness). Hata hivyo, hii si mara ya kwanza kwa Grok kuzua utata. Hapo awali, mfumo huu umewahi kutoa majibu yaliyoegemea kwenye nadharia za njama za mrengo wa kulia, kama vile kudokeza kuwa idadi ya wahanga wa mauaji ya Holocaust ya Wayahudi huenda ilichakachuliwa.

The copyright for this content belongs to the copyright holder or provider. Unauthorized use may result in legal liability under copyright laws and other regulations.