Mlipuko mkubwa umetokea katika kiwanda kimoja cha kemikali kilichoko katika Mkoa wa Shandong, Mashariki mwa China, na kusababisha vifo vya watu watano hadi sasa.
Shirika la habari la NHK la Japan na Shirika la Habari la China Xinhua, pamoja na vyombo vingine vya habari vya ndani, vimeripoti kuwa mlipuko huo ulitokea saa 11:57 asubuhi kwa saa za huko katika kiwanda cha kemikali cha Gaomi, Mkoa wa Shandong. Hadi sasa, imethibitishwa kuwa watu 5 wamepoteza maisha, 19 wamejeruhiwa, na wengine 6 hawajulikani walipo.
Video zilizochukuliwa muda mfupi baada ya mlipuko zinaonyesha moshi mwingi ukitoka kwenye kiwanda hicho, huku madirisha ya majengo yaliyokuwa karibu yakivunjika vipande vipande kutokana na nguvu ya mlipuko.
Kulingana na vyombo vya habari vya ndani, kiwanda hicho kinazalisha dawa za kuulia wadudu na dawa za matibabu, na kina takriban wafanyakazi 300.
Hadi sasa, chanzo halisi cha mlipuko huo bado hakijajulikana, na polisi pamoja na wazima moto wanaendelea na uchunguzi ili kubaini kilichosababisha ajali hiyo.