Katika hatua muhimu ya kukuza uhusiano wa kibiashara na Bara la Afrika, serikali ya China imetangaza mpango kabambe wa kuondolea ushuru wa forodha bidhaa zote kutoka nchi 53 za Kiafrika zenye uhusiano wa kidiplomasia nayo. Tangazo hili, ambalo linaonekana kama mkakati wa China kujenga ushirikiano imara dhidi ya sera za kibiashara za upande mmoja za Marekani, linatarajiwa kufungua milango ya fursa kubwa za kiuchumi kwa bara la Afrika, hasa kwa wakulima wa kahawa.
Idara Kuu ya Forodha ya China (Heiguanzongshu) ilithibitisha sera hii mpya na kusisitiza kuwa lengo ni "kutumia soko kubwa la China ili kuwezesha maendeleo ya pamoja na nchi washirika." Hii ni habari njema hasa kwa nchi zinazozalisha kahawa kwa wingi barani Afrika, ikiwemo Tanzania, Ethiopia na Kenya. Bara la Afrika linachangia takriban asilimia 12 ya uzalishaji wote wa kahawa duniani.
Umuhimu wa soko la China kwa kahawa ya Afrika umekuwa ukiongezeka kwa kasi. Ripoti zinaonyesha kuwa mwaka 2023 pekee, China iliingiza kahawa kutoka Afrika yenye thamani ya dola milioni 170 (takriban Shilingi bilioni 442 za Kitanzania), ikiwa ni ongezeko la asilimia 41.9 ikilinganishwa na mwaka 2014. Hii inadhihirisha kiu inayokua ya kinywaji hicho miongoni mwa Wachina.
Kabla ya sera hii mpya, China ilikuwa ikitoza ushuru wa forodha wa takriban asilimia 8 kwa baadhi ya nchi za Afrika kwa kahawa isiyochomwa (green beans). Kuondolewa kwa ushuru huu kutakuwa na manufaa ya moja kwa moja kifedha. Kwa mfano, kwa tani moja ya kahawa ghafi inayouzwa kwa dola 4,000 (kama Shilingi milioni 10.4), wakulima na wauzaji nje wataepuka kulipa ushuru wa dola 320 (kama Shilingi 832,000) na kodi ya ongezeko la thamani (VAT) ya dola 41.2 (kama Shilingi 107,000). Hii itafanya kahawa ya Afrika kuwa na bei shindani zaidi katika soko la China.
Fursa hii inakuja wakati muafaka, kwani soko la kahawa nchini China linakua kwa kasi ya ajabu. Ripoti ya ‘Maendeleo ya Kahawa Mijini China’ inaeleza kuwa mwaka jana, ukubwa wa sekta ya kahawa nchini humo ulifikia Yuan bilioni 313.3 (zaidi ya Shilingi trilioni 112 za Kitanzania), ikiwa ni ukuaji wa asilimia 18.1 kutoka mwaka uliotangulia. Hivyo, sera hii ya ushuru sifuri inatoa fursa ya dhahabu kwa nchi za Afrika, ikiwemo Tanzania, kuongeza mauzo yake, kuboresha maisha ya wakulima, na kuimarisha uchumi wake kupitia zao la kahawa.