Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu, Yanga SC, wamerejea nchini wakijiamini, huku viongozi wao wakitamba kuwa wameridhishwa na kikosi kipya walichokisuka kwa ajili ya msimu ujao wa mashindano. Kauli hiyo imekuja kufuatia ushindi mnono wa mabao 3-1 walioupata dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa uliofanyika Kigali, Ijumaa iliyopita, ikiwa ni sehemu ya Tamasha la Rayon Sports Day.
Wakizungumza jana jijini Dar es Salaam, Rais wa Yanga, Injinia Hersi Said, na Makamu wake, Arafat Haji, walisema kwa pamoja kuwa mchezo huo umewapa picha nzuri ya uwezo wa wachezaji wapya na mwelekeo wa kocha mpya, Romain Folz. Mshambuliaji mpya, Andy Boyeli, alifungua akaunti yake ya mabao, huku Pacome Zouzoua na nahodha Bakari Mwamnyeto wakikamilisha ushindi huo.
"Tumeridhishwa na viwango vya wachezaji wetu wote wapya. Mechi ile ilikuwa sehemu ya maandalizi na ililenga kuwapa fursa ya kuzoeana na mfumo wa timu. Pamoja na kuwa ni mapema, wameonyesha uwezo mkubwa na kocha mpya naye ametutia moyo," alisema Arafat Haji. Alisisitiza kuwa malengo ya klabu yapo pale pale: kutetea mataji yote ya ndani na kufanya vizuri zaidi kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.
Hersi Said aliongeza kuwa ingawa bado timu haijafikia muunganiko kamili, alifurahishwa na jinsi wachezaji walivyopambana na kudumisha falsafa ya Yanga ya kupigania ushindi katika kila mchezo. Mchezo huo uliwapa fursa mashabiki kuwaona kwa mara ya kwanza wachezaji wapya kama Mohamed Doumbia, Moussa Balla Conte, na Celestin Ecua.
Alipoulizwa kuhusu mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya watani wao wa jadi, Simba, Arafat Haji alionyesha kutokuwa na presha, akisema Yanga imeandaliwa kwa ajili ya mashindano yote na si mechi moja tu. "Tumeiandaa timu yetu kwa ajili ya msimu mzima, si kucheza na Simba tu. Tuko tayari kucheza na yeyote tutakayepangiwa naye," alisema Arafat. Ujumbe huu unaonekana kama salamu kwa washindani wao kuwa Yanga wako tayari kwa vita ya kutetea ubingwa wao.