Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa, CPA Amos Makalla, amesema yuko tayari kupokea matusi kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika jitihada zake za kukitetea chama hicho na kuhakikisha kinakubalika kwa wananchi.
CPA Makalla aliyasema hayo leo kwenye uwanja wa Mwembetogwa, Iringa, alipokuwa akihitimisha ziara yake ya siku tatu katika mikoa ya Mbeya na Iringa.
"Sisi tunawaacha kesho mfurahie vituko, lakini ninajua mkutano wao kesho utakuwa ni kumtukana tu Makalla," alisema.
"Niko tayari kubeba matusi kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), lakini kukitetea na kuwa na chama ambacho kinakubalika kwa wananchi, kuwapelekea sera nzuri za CCM, hiyo ndiyo kazi ya uenezi," aliongeza.
"Leteni tu mawe, nipo tayari, na kesho mtashuhudia Makalla. Kama watawaudhi, kaeni nyumbani, lakini ninajua habari ya kesho ni hiyo, na mimi nipo tayari kwa sababu ndiyo kazi yangu hiyo," alisema.
Makalla aliwaambia wananchi kuwa endapo watakuja na kauli mbiu ya "no reform," tayari ameshaeleza mabadiliko mengi yaliyofanywa.