Mamlaka nchini Ugiriki zimeagiza kusitishwa kwa lazima kwa baadhi ya shughuli za kazi katika maeneo yanayotarajiwa kukumbwa na joto kali linalozidi nyuzi joto 40 Selsiasi tarehe 7 Julai. Wimbi hili la joto linatarajiwa kuendelea hadi tarehe 10 Julai.
Wizara ya Kazi ya Ugiriki imetoa amri ya kusitisha kazi za mikono za nje na huduma za usafirishaji wa chakula kuanzia saa sita mchana hadi saa kumi na moja jioni (saa za huko). Amri hii inatekelezwa zaidi katika maeneo ya Ugiriki ya kati na visiwa mbalimbali. Waajiri pia wamehimizwa kutoa fursa za kufanya kazi wakiwa nyumbani.
Hata hivyo, amri hizi za dharura hazitekelezwi katika mji mkuu wa Athens. Joto hili kali nchini Ugiriki halionekani kuwa la kawaida, kwani Ulaya nzima inakumbwa na joto kali linaloendelea.
Mamlaka za Ugiriki zimesema zinachukua hatua za muda mrefu kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwemo kupeleka idadi kubwa zaidi ya wazima moto katika historia ya nchi hiyo msimu huu wa kiangazi.