Hali ya taharuki na sintofahamu imetawala katika Stesheni ya Treni ya Dodoma baada ya mamia ya wasafiri, zaidi ya 700, waliokuwa wakielekea mikoa ya Tabora, Mpanda na Kigoma, kujikuta wakikwama kwa takriban saa 18. Adha hiyo ilianza baada ya safari yao kusitishwa ghafla kufuatia ajali iliyoihusisha treni ya matengenezo katika eneo la Kintinku, wilayani Manyoni mkoani Singida.
Abiria hao, ambao waliwasili Dodoma majira ya saa mbili usiku wa jana, walijikuta katika mazingira magumu huku wakiwa hawana taarifa rasmi kuhusu hatma ya safari yao. Uvumilivu uliwashinda pale ambapo ahadi za kuondoka zilivyokuwa zikiyeyuka, kuanzia saa saba za usiku hadi alfajiri, bila dalili yoyote ya kuanza safari. Hali hiyo ilichochea hasira na kuwalazimu abiria hao, wakiwemo wanawake na watoto wadogo, kuunda kundi na kuandamana hadi katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mheshimiwa Rosemary Senyamule, ili kufikisha kilio chao.
Mmoja wa abiria, Ashura Madaraka, alieleza kwa uchungu, "Tangu jana usiku tuko hapa, tuliahidiwa tutaondoka saa saba usiku lakini haikuwa hivyo. Hadi asubuhi ndipo stesheni masta anakuja kutuambia tusubiri. Je, tutasubiri hadi lini? Huduma muhimu kama vyoo hazipatikani, na zile zilizopo ni za kulipia."
Malalamiko hayo yaliungwa mkono na Imani Sadiki, ambaye aliongeza kuwa hali imekuwa ngumu zaidi kutokana na gharama zisizotarajiwa. "Inakuwaje tunalazimika kulipa Shilingi 500 kwa ajili ya choo wakati hatukujiandaa kwa hili? Ingawa shirika limesema litagharamia chakula, bado kuna changamoto nyingi, hasa kwa sisi tulio na watoto wadogo," alisema.
Akithibitisha kutokea kwa kero hiyo, Stesheni Masta wa Dodoma, Festo Mgomapayo, alikiri kuwa abiria hao walikwama kutokana na ajali ya treni ya matengenezo iliyokuwa ikifanya kazi zake maeneo ya Kintinku. Hatimaye, baada ya shinikizo na ufuatiliaji, abiria hao waliruhusiwa kuendelea na safari yao majira ya saa nane mchana, wakimaliza saa 18 za mateso na kusubiri kusiko na uhakika.