Hali ya simanzi na mshtuko imetanda katika Ukanda wa Gaza baada ya madaktari katika hospitali ya Nasser iliyoko Khan Younis, kusini mwa eneo hilo, kutoa madai mazito kwamba miili mingi kati ya 90 ya Wapalestina iliyorejeshwa na Israel inaonyesha dalili za wazi za mateso makali na mauaji ya kinyama. Miili hiyo ilikabidhiwa kwa maafisa wa afya wa Gaza kupitia Kamati ya Kimataifa ya Msalaba Mwekundu (ICRC) kama sehemu ya makubaliano tete ya usitishaji vita.
Madaktari waliopokea miili hiyo walieleza kuwa hali waliyoikuta ilikuwa ya kutisha. Walibainisha kuwa miili mingi ilikuwa imefungwa vitambaa machoni, mikono yao ikiwa imefungwa kwa nyuma, na wengi walikuwa na majeraha ya risasi yaliyopigwa kichwani kwa ukaribu, hasa katikati ya macho. Hali hii imeibua hisia kali na madai kwamba watu hao walikamatwa wakiwa hai na kisha kuuawa kimakusudi.
Daktari Ahmad al-Farra, mkuu wa idara ya watoto katika hospitali ya Nasser, aliliambia gazeti la The Guardian la Uingereza kuwa ushahidi unaonyesha waziwazi vitendo vya mateso na mauaji ya papo kwa papo. "Karibu miili yote tuliyoipokea ilikuwa imefungwa macho na mikono. Wengi walikuwa wamepigwa risasi moja kwa moja katikati ya macho. Hizi ni dalili zote za mauaji ya kimfumo," alisema Dk. al-Farra. Aliongeza kuwa ngozi za marehemu hao zilikuwa na michubuko na alama za kupigwa vikali kabla ya vifo vyao, na baadhi ya miili ilionekana kuharibiwa hata baada ya watu hao kupoteza maisha.
Kinachoongeza uchungu zaidi kwa familia ni kitendo cha Israel kurejesha miili hiyo bila utambulisho wowote. Badala ya majina, kila mwili ulikuwa na namba ya usajili, na hivyo kuacha jukumu zito la utambuzi kwa familia zenye ndugu waliopotea. Dk. al-Farra alieleza kuwa hospitali zao zilizoharibiwa na vita hazina vifaa vya kufanya uchunguzi wa vinasaba (DNA), na anahisi Israel inafanya hivi kimakusudi ili kuongeza mateso kwa familia.
Madai haya mazito yanakuja wakati ambapo mchakato wa kubadilishana miili kati ya Israel na kundi la Hamas umekuwa kikwazo kikubwa katika utekelezaji wa makubaliano ya usitishaji vita. Chini ya makubaliano hayo, Hamas inatakiwa kuirejesha Israel miili ya mateka waliokufa, na kwa upande wake, Israel inarejesha miili ya Wapalestina waliouawa vitani. Hata hivyo, mivutano imeibuka, ambapo Israel ilisitisha kwa muda uingizaji wa misaada ya kibinadamu Gaza ikidai Hamas inachelewesha urejeshaji wa miili ya mateka.
Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF), lilipoulizwa na gazeti la The Guardian kuhusu madai haya ya mateso, lilijibu kuwa suala hilo liko chini ya mamlaka ya Idara ya Magereza ya Israel (IPS) na halikutoa maelezo zaidi.