Muda wa mapumziko umekwisha kwa Wekundu wa Msimbazi, Simba SC, ambao jana wamerejea rasmi kambini katika viunga vya Mo Arena, Bunju, kujiandaa na kipindi kigumu na muhimu mbele yao. Baada ya mapumziko mafupi ya siku tatu yaliyotolewa na kocha Fadlu Davids, sasa ni mwendo wa kazi mfululizo bila kupumzika hadi baada ya mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Kikosi hicho kinakabiliwa na ratiba ngumu ya michezo mitatu mikubwa katika siku kumi. Mwanzo ni tamasha kubwa la klabu, Simba Day, litakalofanyika Septemba 10 kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa. Katika kilele hicho, Simba watapambana na Gor Mahia kutoka Kenya, huku wakitambulisha rasmi kikosi chao kamili cha msimu wa 2025/26 mbele ya maelfu ya mashabiki wao.
Siku sita baadaye, yaani Septemba 16, macho na masikio yote ya Watanzania yataelekezwa uwanjani hapo tena, ambapo Simba itachuana na watani wao wa jadi, Yanga, katika mchezo wa Ngao ya Jamii. Huu ni mchezo wa heshima na kiashiria cha ufunguzi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, na Simba wamedhamiria kuanza msimu kwa kuwachapa wapinzani wao.
Kibarua hakitaishia hapo. Mara baada ya dabi hiyo, kikosi cha Simba kitasafiri kuelekea Botswana kwa ajili ya mchezo wa kwanza wa hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Gaborone United, utakaopigwa Septemba 20.
Akizungumzia ratiba hiyo ngumu, Kocha Mkuu Fadlu Davids, alionyesha kujiamini akisema kuwa ameandaa kikosi chake sio tu kimchezo bali pia kisaikolojia kuhimili presha ya kucheza mechi kila baada ya siku tatu na kusafiri umbali mrefu. "Nimejiandaa kwa wingi wa mechi tutakazocheza. Hakuna muda wa kujiuliza wala kuhuzunika, ni kuingia uwanjani na kupambana tu," alisema kocha huyo mwenye uzoefu.
Wakati timu ikijiandaa uwanjani, uongozi nao haukulala. Jana, klabu hiyo ilifanya uzinduzi wa kuvutia wa jezi zao mpya za msimu wa 2025/26. Hafla hiyo iliyofanyika Masaki jijini Dar es Salaam, ilihudhuriwa na watu mashuhuri, akiwemo Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, aliye kuwa mgeni rasmi, kuashiria kuwa klabu iko tayari kupambana ndani na nje ya uwanja.