Serikali imetoa ahadi thabiti ya kushirikiana na wadau wote ili kuhakikisha mchezo wa kuogelea kwa watu wenye ulemavu unapata msukumo mpya na kustawi kuanzia ngazi ya shule hadi kwenye jamii. Kauli hiyo imetolewa kama ishara ya matumaini mapya, wakati wa tamasha maalum la kusaka na kuibua vipaji chipukizi lililofanyika katika bwawa la Shule ya Sekondari ya Shaaban Robert jijini Dar es Salaam.
Tukio hilo la aina yake, lililoandaliwa na Chama cha Kuogelea kwa Watu Wenye Ulemavu Tanzania (TPSA), lilileta pamoja waogeleaji 102 kutoka klabu na shule 11, likionesha wazi kuwa kuna hazina kubwa ya vipaji inayohitaji kuendelezwa. Akizungumza kwa niaba ya serikali, Afisa Mwandamizi kutoka Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Charles Maguzu, alisema serikali iko tayari kuunga mkono jitihada zote zinazolenga kukuza michezo jumuishi nchini.
"Ili kufikia lengo la 'michezo kwa wote', ni lazima tuunganishe nguvu. Tunakipongeza sana Chama cha TPSA kwa kuandaa tamasha hili. Uwepo wa washiriki wengi kutoka shuleni unatupa moyo, na sisi kama serikali tutahakikisha tunatoa ushirikiano ili kuona watu wengi zaidi wenye ulemavu wanashiriki kikamilifu," alieleza Maguzu. Aliongeza kwa kutoa wito kwa wazazi na walezi wenye watoto wenye mahitaji maalum, kuwatia moyo na kuwapa fursa za kushiriki kwenye michezo ili waonyeshe uwezo wao.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa TPSA, Ramadhan Namkomveka, alieleza kuwa lengo kuu la tamasha hilo lilikuwa ni kutambua waogeleaji wapya watakaojenga msingi wa timu imara ya taifa ya baadaye. Alisema michezo hii inalenga kujenga stadi, kuongeza ushiriki, na kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa michezo kwa afya na maendeleo ya watu wenye ulemavu.
Baadhi ya klabu na shule zilizong'arisha tamasha hilo ni pamoja na Genesis School, Jaffery Academy, Josephian School, Pugu Secondary School, Jangwani Secondary School, Down Syndrome Tanzania, na Almuntazir Islamic School.