Akitumia jukwaa la uzinduzi wa kampeni zake za kitaifa jijini Tanga, mgombea urais kupitia chama cha National League for Democracy (NLD), Bwana Doyo Hassan Doyo, ameweka bayana misingi mikuu sita itakayotumika kama dira ya serikali yake endapo wananchi watampa ridhaa ya kuongoza nchi. Alisema chama chake kimejipanga kwa mikakati madhubuti kuhakikisha Tanzania inafikia maendeleo jumuishi.
Akihutubia mamia ya wafuasi wake, Doyo alieleza kuwa lengo kuu la NLD ni kujenga uchumi imara unaotokana na uzalishaji wa ndani, huku ukihakikisha haki, ustawi na usawa vinamfikia kila Mtanzania. Ili kufikia ndoto hiyo, alifafanua kuwa uongozi wake utasimama imara kwenye nguzo sita muhimu.
Nguzo ya kwanza ni Uzalendo, haki na usawa, ambapo serikali yake itahakikisha kila raia anapata haki sawa bila ubaguzi. Pili, ni Uwajibikaji na uongozi wa kimaadili, akiahidi viongozi watakaowajibika kwa wananchi na kuzingatia maadili ya taifa. Tatu, alitaja Uwezeshaji wa wananchi kiuchumi na kijamii kama kipaumbele, akilenga kuwatoa wananchi kutoka lindi la umasikini.
Aidha, Doyo alisisitiza juu ya Kulinda na kuongeza thamani ya rasilimali za Taifa ili zinufaishe kizazi cha sasa na vijavyo. Nguzo ya tano ni Ujenzi wa taasisi imara zitakazofanya kazi kwa weledi na kuwajibika kwa umma. Mwisho, aliahidi Maendeleo endelevu yatakayozingatia utunzaji wa mazingira na matumizi sahihi ya teknolojia ya kisasa.
Katika hotuba yake, Doyo aligusa hisia za wengi aliposema, “Nchi yetu siyo masikini, lakini sisi tunaitwa wanyonge. Sasa ili msiitwe wanyonge, msifanye mchezo, changamkeni Oktoba 29, nendeni mnichague Doyo Hassan Doyo.” Aliahidi kuwa serikali yake itakuwa suluhisho la changamoto zilizopo na itahakikisha utajiri wa nchi unawanufaisha wananchi wote.