Wawakilishi kutoka Marekani na Urusi wamefanya mkutano wa pili kwa ajili ya kujadili kurejesha hali ya kawaida katika ofisi zao za kidiplomasia. Mkutano huo ulidumu kwa takriban saa sita na ulifanyika nchini Uturuki, katika ubalozi mdogo wa Urusi uliopo Istanbul.
Kwa mujibu wa shirika la habari la RIA Novosti na vyanzo vingine, ujumbe wa Marekani uliondoka kwenye ofisi za ubalozi mdogo wa Urusi baada ya kukaa kwa takriban saa sita tangu walipowasili.
Ujumbe wa Urusi uliongozwa na Balozi wa Urusi nchini Marekani, Bwana Aleksandr Darchiyev. Kwa upande wa Marekani, ujumbe huo uliongozwa na Bi Sonata Coulter, Naibu Katibu Msaidizi wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani anayeshughulikia masuala ya Urusi na Ulaya ya Kati.
Katika mazungumzo hayo, pande hizo mbili zilijadili masuala mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kurejesha utendaji wa kawaida wa ofisi za kidiplomasia, kuanzisha tena safari za ndege kati ya nchi hizo mbili, na kurejesha mali za Urusi zilizozuiliwa nchini Marekani.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilitoa taarifa ikisema kuwa mazungumzo hayo yaliendeleza "mbinu yenye kujenga" iliyoanzishwa katika mkutano wa kwanza. Pia, walikubaliana kuendelea kujadili kuhusu kuhakikisha huduma za kibenki zinazotegemeka kwa ofisi zao za kidiplomasia na kubadilishana hati zinazohusika.
Marekani ilielezea tena wasiwasi wake kuhusu hatua ya Urusi ya kupiga marufuku uajiri wa wafanyakazi wa ndani katika ubalozi wao, ikisema kuwa hatua hiyo ni "kikwazo kikubwa katika kudumisha kiwango cha wafanyakazi imara na endelevu katika ubalozi wa Marekani mjini Moscow."
Pande hizo mbili zilikubaliana kujadili uwezekano wa kufanya mikutano mingine katika siku za usoni, kadri itakavyohitajika. Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilieleza kuwa tarehe, mahali, na wajumbe wa mikutano hiyo ya baadaye bado hayajaamuliwa.
Balozi wa Urusi nchini Marekani, Bwana Darchiyev, aliliambia shirika la habari la serikali la TASS kuwa mkutano huo ulifanyika katika "mazingira mazuri." Alieleza kuwa pande hizo mbili zilikubaliana kurahisisha kanuni zinazohusu usafiri wa kidiplomasia na utoaji wa viza kwa mabalozi wa nchi nyingine.
Alisisitiza pia kuwa "walipa kipaumbele suala la kurejesha haraka mali za kidiplomasia za Urusi ambazo zimezuiwa na mamlaka za Marekani." Aliongeza kuwa ujumbe wa Urusi ulipendekeza kuanzishwa tena kwa safari za ndege kati ya Moscow na Washington.
Urusi ilikuwa imeomba kuanzishwa tena kwa safari za ndege za moja kwa moja katika mkutano wa kwanza uliofanyika Istanbul mnamo Februari 27.
Marekani ilisitisha safari za ndege za moja kwa moja kuelekea Urusi mnamo Februari 2022, baada ya Urusi kuivamia Ukraine. Balozi za nchi hizo mbili zimekuwa zikifanya kazi kwa wafanyakazi wachache kwa miaka kadhaa kutokana na kufukuzwa kwa wanadiplomasia.
Inaarifiwa kuwa suala la Ukraine halikujadiliwa katika mkutano huu.
Hapo awali, Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilisisitiza kuwa mkutano huu unalenga tu uhusiano wa pande mbili kati ya Marekani na Urusi, na masuala yanayohusiana na Ukraine hayakuingizwa kwenye ajenda.
Siku hiyo hiyo, pande hizo mbili zilibadilishana wafungwa katika mji wa Abu Dhabi, Falme za Kiarabu (UAE). Urusi ilimwachilia raia mwenye uraia pacha wa Marekani na Urusi, ambaye alikuwa amehukumiwa kifungo cha miaka 12 kwa kosa la uhaini baada ya kutoa mchango kwa shirika la hisani linalohusika na Ukraine lenye makao yake makuu Marekani.
Marekani ilimwachilia raia mwenye uraia pacha wa Ujerumani na Urusi mnamo 2023, ambaye alikuwa amezuiliwa huko Cyprus. Inadaiwa kuwa alishtakiwa kwa kusafirisha vifaa nyeti vya kielektroniki vya Marekani.