Serikali ya Israeli imekiri kufanya "kosa la kutisha" baada ya vikosi vyake vya ardhini kufanya shambulio la kinyama kwa kutumia kifaru dhidi ya Hospitali ya Nasser, hospitali pekee ya umma iliyokuwa bado inafanya kazi kusini mwa Gaza. Shambulio hilo limesababisha vifo vya watu wasiopungua 20, wakiwemo waandishi wa habari na wafanyakazi wa afya, na kuzua ghadhabu kali kutoka kwa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (Arab League) na serikali ya Misri.
Kinyume na ripoti za awali zilizodhani ni shambulio la angani, kituo cha runinga cha serikali ya Israeli, Kan TV, kimefichua kuwa shambulio hilo lilitekelezwa na kifaru cha jeshi la ardhini. Kituo hicho, kikiwanukuu makamanda wa jeshi, kilidai kuwa kifaru hicho kilikuwa kinalenga kamera za ulinzi ambazo Hamas walikuwa wameziweka kwenye jengo la hospitali hiyo kwa ajili ya kupeleleza mienendo ya jeshi.
Wizara ya Afya ya Gaza imeripoti kuwa miongoni mwa waliopoteza maisha ni waandishi wa habari watano na wahudumu wa afya wanne. Shambulio la pili lililenga eneo hilo hilo wakati waokoaji walipokuwa wakijaribu kuhamisha majeruhi. Hii inaongeza idadi ya waandishi wa habari waliouawa tangu kuanza kwa vita kufikia 273, kwa mujibu wa takwimu za wizara hiyo.
Shambulio hili limechochea hasira katika ulimwengu wa Kiarabu. Katibu Mkuu wa Arab League, Ahmed Aboul Gheit, alilaani shambulio hilo akiliita "uovu mwingine katika mfululizo wa mauaji ya kinyama yanayofanywa na jeshi la Israeli dhidi ya raia." Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri nayo ilitoa taarifa kali, ikikitaja kitendo hicho kama "sura mpya ya uvunjaji wa sheria za kimataifa za kibinadamu na uchokozi wa wazi wa Israeli."
Kutokana na lawama hizo kali, Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu alitoa taarifa akisema Israeli inajutia tukio hilo na kwamba uchunguzi wa kina unafanywa. Hata hivyo, msemaji wa jeshi la Israeli, Efi Defrin, alijaribu kuihamishia lawama kwa Hamas, akidai kuwa kundi hilo linatengeneza "mazingira yasiyowezekana" kwa jeshi kufanya operesheni zake kwa kujificha miongoni mwa raia.
Tukio hili limetokea huku Israeli ikiendelea kuwazuia waandishi wa habari wa kigeni kuingia Gaza, na hivyo kuwaacha wanahabari wa ndani na wa Kiarabu pekee katika hatari kubwa ya kuripoti matukio ya vita kutoka eneo la tukio.