Jeshi la Polisi Mkoani Shinyanga limechukua hatua kali dhidi ya madereva watatu waliobainika kuendesha magari kwa mwendo kasi unaozidi kiwango kinachoruhusiwa kisheria. Madereva hao wamefungiwa leseni zao kwa muda wa miezi mitatu kila mmoja baada ya kukutwa wakiendesha kati ya kilomita 100 hadi 118 kwa saa, kinyume na kanuni za usalama barabarani. Hatua hii imetangazwa leo Julai 23, 2025, na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Janeth Magomi, wakati akitoa taarifa ya utendaji kazi kwa vyombo vya habari, ikihusisha kipindi cha kuanzia Juni hadi Julai 22, mwaka huu.
Kamanda Magomi alifafanua kuwa katika kipindi hicho, kikosi cha usalama barabarani kimefanikiwa kukamata makosa 5,759 ya usalama barabarani. Kati ya makosa hayo, 4,557 yalihusisha magari, na ndipo madereva hao watatu waliofungiwa leseni zao walipobainika. Aliongeza kuwa upande wa pikipiki na bajaji, jumla ya makosa 1,202 yalibainika. Madereva wengine waliokamatwa kwa makosa mbalimbali, wakiwemo wa magari, waliwajibishwa kwa kulipa faini za papo hapo.
Mbali na masuala ya usalama barabarani, Kamanda Magomi pia alifafanua kuwa jeshi hilo limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa 125 kwa makosa mbalimbali ya uhalifu. Watuhumiwa hao walikutwa na vielelezo muhimu ikiwemo gramu 2,261 za bangi, lita 142 za pombe ya moshi (gongo), kilo 29 za mirungi. Pia walikamatwa na vifaa mbalimbali vya wizi ikiwemo bajaji moja, televisheni saba, mabati 16, nondo 17, vitanda vinne, redio nane, na pikipiki 22.
Katika jitihada za kuendelea kuhamasisha umma kuhusu umuhimu wa kufuata sheria, Jeshi la Polisi Shinyanga limeendesha mikutano 64 ya kutoa elimu kwa wananchi, wadau mbalimbali, na madereva wa vyombo vya moto. Kampeni hizi zina lengo la kuhimiza uzingatiaji wa sheria na kanuni za usalama barabarani, na pia kutoa ufahamu kuhusu athari za uhalifu, ili kujenga jamii salama na yenye utii wa sheria. Hatua hizi zinaonesha dhamira ya Jeshi la Polisi Shinyanga katika kudhibiti uhalifu na kuhakikisha usalama wa barabarani unaimarika kwa manufaa ya Watanzania wote.