Yanga SC imeongeza ushindani katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Mashujaa FC katika mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa KMC, Kinondoni, Dar es Salaam. Ushindi huo umeifanya Yanga kurudi kwenye vita ya nafasi ya juu ya msimamo wa ligi.
Kwa sasa, Azam FC inaongoza ligi ikiwa na pointi 33 baada ya michezo 15. Simba SC inashika nafasi ya pili na pointi 31 kwa michezo 12, huku Yanga ikiwa na pointi 30 katika idadi hiyo hiyo ya michezo, ikifuatwa na Singida Black Stars yenye pointi 30 lakini ikiwa imeshacheza mechi 14, ikizidiwa uwiano wa mabao na Yanga.
Katika mchezo wa leo, Prince Dube alikuwa nyota wa mchezo baada ya kufunga mabao yote matatu (hat-trick), ikiwa ni hat-trick ya kwanza kufungwa msimu huu wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2024/25. Mashujaa walipata mabao yao kupitia David Ulomi na Idrisa Stambuli.
Ushindi huo wa Yanga umeongeza ushindani mkali katika nafasi tatu za juu, na vita ya ubingwa inatarajiwa kuwa kali zaidi katika mechi zijazo, huku mashabiki wakisubiri kwa hamu kuona jinsi miamba hiyo mitatu itakavyopambana kusalia kileleni mwa msimamo wa ligi.