Katika harakati za mwisho za kampeni za Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mgombea urais wa Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), Salum Mwalimu, amejielekeza kwa kundi la wajasiriamali wadogo na wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi, akiahidi kuwalinda dhidi ya usumbufu na bughudha kutoka kwa mamlaka.
Akizungumza eneo la Saranga, Kibamba, karibu na kituo kikuu cha mabasi cha Mbezi Mwisho jijini Dar es Salaam, Mwalimu aliwahakikishia wapigadebe, wabeba mizigo, na wajasiriamali wengine kuwa serikali yake haitawaruhusu waondolewe kwenye maeneo yao ya kutafutia riziki bila kuandaliwa fursa mbadala. Alisema sera yake kuu ni kulinda kila Mtanzania anayejitafutia maisha kihalali.
"Mimi nikiwa rais wa nchi hii, mtu yeyote anayejitafutia riziki kihalali nitataka aachwe asibughudhiwe," alisema Mwalimu na kuongeza, "Sera yangu ni kwamba, kukuondoa hapo ina maana nimekutengenezea mahali pengine pazuri zaidi. Hamtasumbuliwa mpaka pale nitakapowatengenezea fursa nyingine."
Hata hivyo, aliweka wazi kuwa ulinzi huo utawahusu wale tu wanaofanya biashara halali. "Ilimradi hauuzi bangi, dawa za kulevya au kujihusisha na shughuli yoyote haramu, hautaguswa. Wewe fanya kazi zako kwa uhuru," alisisitiza mgombea huyo wa CHAUMMA.
Ahadi hii inakuja kama faraja kwa maelfu ya vijana wanaojiajiri katika sekta isiyo rasmi, ambao mara kwa mara hujikuta katika mikwaruzano na vyombo vya dola. Mwalimu anatumia sera hii kujipambanua kama mtetezi wa "watu wa chini" katika kinyang'anyiro cha urais.