Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewatakia Waislamu wote heri ya mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan huku akisisitiza umuhimu wa kudumisha amani na kuiombea nchi. Kupitia ujumbe alioutoa katika mtandao wa kijamii wa X, Rais Samia aliwataka wananchi kuendeleza ibada kwa uadilifu na kumwomba Mwenyezi Mungu awape baraka na uongozi mwema katika kipindi hiki.
"Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema atuongoze na kutusimamia kwenye ibada hii muhimu katika imani, aipe kibali cha kheri na kuipokea," aliandika Rais Samia.
Aidha, aliwasihi Watanzania wote, bila kujali nafasi zao, kutekeleza majukumu yao kwa haki na uadilifu kwa manufaa ya taifa. "Tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu atujalie kila mmoja kwa nafasi yake kuendelea kutekeleza wajibu wake kwa uadilifu, kwa haki na kweli na matokeo ya maisha na kazi zetu yawe yenye kumpendeza yeye, na yenye kulifaa taifa letu na watu wake. Ramadhan Mubarak," aliongeza.
Viongozi wengine wa serikali pia walitoa salamu zao kwa Waislamu. Makamu wa Rais, Dk. Philip Mpango, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, na Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba, walitumia mitandao ya kijamii kuwatakia Waislamu mfungo mwema na kuhimiza mshikamano wa kitaifa.
Majaliwa, akimwakilisha Rais Samia katika maombi ya kitaifa yaliyoandaliwa na Umoja wa Viongozi wa Makanisa jijini Dar es Salaam, alisisitiza umuhimu wa maombi kwa ajili ya taifa na viongozi wake. Alisema kuwa bila amani na utulivu, maendeleo ya kiuchumi hayawezi kupatikana.
"Nchi haiwezi kuwa na uhuru wa kuabudu, pasipo amani hatuwezi kufanya shughuli za uzalishaji mali. Katika eneo hili ninawapongeza na kuwashukuru madhehebu yote ya dini kwa kuendelea kuiombea nchi yetu amani, mshikamano na utulivu," alisema Majaliwa.
Dk. Mwigulu Nchemba naye alikumbusha kuwa Ramadhan ni mwezi wa rehema, msamaha na ibada, na akawatakia Waislamu wote mfungo wenye baraka na amani.
Salamu hizi kutoka kwa viongozi wa serikali zinaonesha mshikamano na utambuzi wa umuhimu wa maadili ya kiroho katika kudumisha amani na maendeleo ya taifa.