Samsung inajiandaa kuzindua simu mpya inayokunjwa mara mbili, ambayo itatolewa sambamba na simu za Galaxy Z Fold na Galaxy Z Flip.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka sekta ya teknolojia, kampuni hiyo inapanga kuanza kupokea vipuri vya simu hiyo mpya kufikia mwezi Aprili mwaka huu. Hii inamaanisha kuwa uzalishaji wa simu hiyo utaanza kwa wakati mmoja na uzalishaji wa Galaxy Z Series, ambazo zinatarajiwa kuzinduliwa rasmi mwezi Julai.
Vyanzo vya ndani vimeeleza kuwa simu hiyo mpya, inayojulikana kama multi-fold phone, inatengenezwa sambamba na Z Series tangu hatua za awali za maendeleo hadi uzalishaji, na hivyo kuna uwezekano mkubwa wa kuzinduliwa kwa pamoja.
Hadi sasa, Samsung imekuwa ikitoa simu za Fold zinazokunjwa kushoto na kulia mara moja, pamoja na Flip zinazokunjwa juu na chini. Hata hivyo, mwaka huu kampuni inaleta aina mpya ya simu inayokunjwa mara mbili, ambayo itapanua chaguzi kwa watumiaji na kubadilisha uzoefu wa matumizi ya simu za foldable.
Hii ni mara ya kwanza kwa Samsung kuzindua simu ya aina hii. Tangu kuzindua Galaxy Fold mnamo 2019 na kufungua soko la simu zinazokunjwa, kampuni imeendelea kuboresha teknolojia hiyo kwa kutoa simu zinazokunjwa mara moja. Kwa kuanzisha teknolojia ya multi-fold, Samsung inalenga kujitofautisha na washindani wake, hasa makampuni ya China yanayoongeza ushindani katika soko hili, pamoja na Apple ambayo inatarajiwa kuingia kwenye soko la simu zinazokunjwa siku za usoni.
Ripoti zinaonyesha kuwa simu hii mpya itakuwa na muundo unaofanana na mfano wa Flex G uliowahi kuonyeshwa na Samsung Display kwenye maonyesho ya teknolojia. Kwa kuzingatia uimara na matumizi bora, Samsung imeamua kutumia mfumo wa in-folding, ambapo skrini hukunjwa kuelekea ndani, huku sehemu ya nje ikiwa na skrini ndogo ya ziada kwa matumizi rahisi.
Simu hiyo itakuwa na skrini kuu (main display) ya inchi 9.96 na skrini ya nje (cover display) ya inchi 6.49, ambayo ni sawa na ukubwa wa skrini za Galaxy Fold SE na Fold 7. Hata hivyo, simu hiyo haitakuwa na digitizer, kipengele kinachowezesha utumiaji wa kalamu ya S-Pen. Uamuzi huu unalenga kupunguza unene wa kifaa, kwani muundo wa kukunjwa mara mbili hufanya simu kuwa nene zaidi ikilinganishwa na Fold na Flip za kawaida.
Kwa kuwa huu ni uzinduzi wa kwanza wa aina hii ya simu, Samsung inatarajiwa kutoa idadi ndogo ya vitengo, takriban 200,000, ili kupima mwitikio wa soko. Mmoja wa wachambuzi wa sekta hiyo alieleza kuwa kampuni hiyo itatumia mkakati sawa na ule uliotumiwa wakati wa uzinduzi wa Fold SE, ambapo simu hizo zilipelekwa kwenye masoko machache kwa majaribio kabla ya uzalishaji mkubwa.