Jibini (cheese) inayotengenezwa kwenye maabara bila kutumia maziwa ya ng'ombe inatarajiwa kuingia sokoni katika miaka michache ijayo, ikiwa ni hatua kubwa katika teknolojia ya chakula. Kampuni ya Uingereza iitwayo 'Better Dairy' inaongoza katika utengenezaji wa jibini hili la kivegani (vegan), ambalo linadaiwa kuwa na ladha inayokaribiana na jibini halisi pamoja na faida za kiafya.
Wataalamu hawa wamefanikiwa kufanya jambo lililoonekana kama la ajabu: kutengeneza protini muhimu ya maziwa iitwayo ‘casein’—ambayo ndiyo msingi wa jibini—bila kumhusisha mnyama yeyote. Mchakato wa jadi unahusisha kuchukua maziwa ya ng'ombe, kutoa protini ya casein, na kuichachisha. Hata hivyo, Better Dairy wanatumia teknolojia ya kijenetiki kuibadilisha chachu (yeast) ili badala ya kutoa pombe wakati wa uchachushaji, itoe protini ya casein. Kisha, casein hiyo huchanganywa na mafuta yatokanayo na mimea pamoja na madini mengine ili kutengeneza ladha na muundo unaofanana na jibini halisi.
Kampuni hiyo imeeleza kuwa tayari imefanya majaribio ya ladha kwa jibini aina ya cheda (cheddar) iliyoikomaza kwa miezi mitatu, sita, na kumi na miwili, na kuthibitisha kuwa ina ladha inayofanana sana na ile ya asili. Hii inatoa matumaini kwa watu wasiotumia bidhaa za wanyama (vegans) ambao wanakosa ladha halisi ya jibini.
Mbali na ladha, jibini hili lina faida kadhaa za kiafya. Kwanza, halina 'lactose' (sukari ya maziwa), hivyo linafaa kwa watu wenye matatizo ya kumeng'enya sukari hiyo. Pili, lina kiwango cha chini cha kolesteroli na mafuta yaliyojaa (saturated fats) ikilinganishwa na jibini la wanyama.
Hata hivyo, kuna changamoto kadhaa kabla ya bidhaa hii kufika mezani pako. Kwanza, kwa kuwa ni "chakula kipya," inahitaji kupitia mchakato mkali wa kuidhinishwa na mamlaka za chakula barani Ulaya ili kuthibitisha usalama wake kwa mlaji. Pili, gharama za uzalishaji kwa sasa ziko juu, na kufanya bei yake kuwa ghali kuliko jibini la kawaida. Hata hivyo, Better Dairy wanatumai kushirikiana na wazalishaji wakubwa ili kupunguza gharama na kufikia bei ya soko ndani ya miaka mitatu hadi minne ijayo.
Kuhusu wasiwasi kwamba ni "chakula kilichosindikwa kupita kiasi," kampuni hiyo inajibu kuwa watu wengi wana taswira isiyo halisi kuhusu uzalishaji wa maziwa. Wanasema sekta ya maziwa tayari ni ya viwandani na jibini lenyewe si "chakula cha asili" bali hupitia usindikaji mwingi.