Watumiaji wa Apple wanatarajia kwa hamu ujio wa kipengele cha kupima shinikizo la damu kwenye Apple Watch, ambacho kinatarajiwa kuletwa kwenye matoleo mapya yatakayozinduliwa mwaka huu. Hata hivyo, kulingana na habari kutoka kwa Mark Gurman wa Bloomberg, huenda kipengele hiki kisipatikane mapema kama inavyotarajiwa kutokana na changamoto za kiufundi zinazoikabili Apple.
Apple inaendelea kufanya majaribio na teknolojia ya kupima shinikizo la damu, na hata imesajili patent mpya inayoonyesha mfumo unaotumia sensa iliyojazwa maji ndani ya kamba ya saa kupima shinikizo la damu. Lakini, mshindani wao mkuu, Samsung, tayari ameshaweka kipengele hiki kwenye saa zake za Galaxy Watch tangu mwaka 2020.
Watumiaji wa Galaxy Watch wameripoti kuwa vipimo vya shinikizo la damu kutoka kwenye saa zao vinafanana kwa karibu na vipimo vinavyotolewa na vifaa vya kawaida vya kupima shinikizo la damu.
Licha ya kuchelewa, Apple inatarajiwa kuzindua Apple Watch Ultra 3 na Apple Watch Series 11 mwezi wa tisa, ambapo huenda kipengele hiki kipya kikapatikana. Hata hivyo, wataalam wanasisitiza kuwa vipimo vya shinikizo la damu kutoka kwenye saa janja bado vinaweza kuwa na tofauti ndogo ikilinganishwa na vifaa vya kawaida, na inashauriwa kutumia saa janja kama chombo saidizi cha kupima shinikizo la damu.