Majira ya alfajiri ya Juni 18, 2025, mji mkuu wa Iran, Teheran, ulishuhudia milipuko mikubwa na midogo iliyotikisa jiji zima, huku kishindo kikuu kikisikika majira ya saa 11 asubuhi. Mashambulizi haya yanakuja mara baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kuitaka Iran “isalimu amri bila masharti.”
Vyombo vya habari vya kimataifa, ikiwemo Shirika la Habari la Associated Press (AP) na Shirika la Habari la Ufaransa (AFP), viliripoti kuwa Israeli ilikuwa imetoa onyo la awali la kushambulia maeneo yenye makazi, vituo vya kijeshi, na makampuni ya kutengeneza dawa, yaliyopo kusini mwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mehrabad, Teheran.
Jeshi la Ulinzi la Israeli lilithibitisha mashambulizi hayo, likisema kuwa “zaidi ya ndege 50 za kivita za Jeshi la Anga la Israeli zimefanya mashambulizi ya angani dhidi ya Teheran katika saa chache zilizopita.” Jeshi hilo lilibainisha kuwa shabaha kuu ilikuwa ni vituo vya uzalishaji wa centrifuge (vifaa vinavyotumika kurutubisha urani) vilivyoko Teheran, kama sehemu ya jitihada pana za kuzuia mpango wa Iran wa kuendeleza silaha za nyuklia.
Waziri wa Ulinzi wa Israeli, Israel Katz, aliandika kwenye mtandao wa X (zamani Twitter) baada ya shambulio hilo: “Kimbunga kinapita Teheran. Hivi ndivyo tawala za kidikteta zinavyoanguka.” Aliongeza kuwa “vituo vya televisheni na malengo mengine, ikiwemo alama za utawala, zimeshambuliwa na kuharibiwa, huku idadi kubwa ya wakazi wakikimbia.”
Saa chache kabla ya shambulio hilo, Rais Trump alikuwa ameitaka Iran “isalimu amri bila masharti,” akipendekeza hata uwezekano wa operesheni ya kumuondoa kiongozi mkuu wa Iran. Iliripotiwa kuwa Trump alifupisha ziara yake ya Mkutano wa Kilele wa G7 kwa siku moja na kurudi haraka Ikulu ya White House, ambapo alifanya mkutano wa Baraza la Usalama wa Kitaifa kujadili uwezekano wa Marekani kuingilia kati mzozo kati ya Israeli na Iran.
Kwa upande wake, Iran imedai kuwa mifumo yake ya ulinzi wa anga imefanikiwa kuzuia mashambulizi ya Israeli. Televisheni ya Taifa ya IRIB ilionesha video ikidai kuonesha droni ya kisasa ya Israeli aina ya Hermes 900 ikidunguliwa katika eneo la Isfahan, katikati mwa Iran, ambako kituo cha nyuklia cha Natanz kipo. Jeshi la Israeli lilithibitisha kuwa droni yake ilianguka nchini Iran baada ya kupigwa na kombora la kutoka ardhini kwenda angani, lakini lilisema hakuna hatari ya kuvuja kwa taarifa muhimu.
Aidha, Iran imedai kudungua ndege tano za kivita aina ya F-35 tangu mapigano yalipoanza Juni 13. Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) kilitangaza kuwa kimetumia kombora la kisasa la Fattah-1 aina ya hypersonic (lenye kasi kubwa sana) katika mashambulizi yake ya hivi karibuni dhidi ya Israeli. Kombora la Fattah-1, ambalo limetengenezwa nchini Iran, lina uwezo wa kuruka umbali wa hadi kilomita 1,400. Mvutano huu unaendelea kuongezeka na unahofia kuleta athari kubwa kwa usalama wa kanda na hata duniani kote.