Angalau watu nane wameripotiwa kufariki baada ya mgodi wa mawe kuporomoka katika kisiwa cha Java nchini Indonesia.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka mashirika ya habari ya AFP na Reuters, ajali hiyo ilitokea majira ya saa tatu na nusu asubuhi (saa za huko) katika mgodi wa chokaa ulioko Cirbon City, jimbo la West Java. Wafanyakazi na mitambo mizito walifukiwa na kifusi cha mgodi ulioanguka.
Polisi wa eneo hilo walithibitisha kuwa miili ya watu nane ilipatikana kutoka kwenye vifusi, na watu wengine kumi na wawili walijeruhiwa na kupelekwa hospitali kwa matibabu.
Hivi sasa, timu za uokoaji zinaendelea na msako kwa kutumia vifaa kama vile tingatinga, zikihofia kuwa kuna watu wengine waliokwama chini ya kifusi.
Inaarifiwa kuwa mgodi huu ulishawahi kuporomoka mara moja hapo awali, mwezi Februari mwaka huu, lakini hakukuwa na majeruhi au vifo vilivyoripotiwa wakati huo.
Gavana wa West Java, Bwana Dedi Mulyadi, amesema kuwa mgodi huo haukuwa ukifuata viwango vya usalama vinavyotakiwa. Ameagiza kufungwa kwa mgodi huo uliohusika na ajali pamoja na migodi mingine yote iliyoko katika eneo hilo ili kuepusha majanga mengine.