Moto Wawaka Yemen: Saudia Yaua Wapiganaji 20, Mipango ya Taifa Jipya la 'Arabia Kusini' Yaanikwa

international | Sat Jan 03 2026


Moto Wawaka Yemen: Saudia Yaua Wapiganaji 20, Mipango ya Taifa Jipya la 'Arabia Kusini' Yaanikwa

Hali ya usalama katika eneo la Ghuba imezidi kuwa tete huku milio ya risasi na mabomu ikitawala anga la Yemen. Katika kile kinachoonekana kama 'ndugu kugombana na kushika mapanga', Muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia umefanya mashambulizi makali ya anga dhidi ya washirika wao wa zamani, Baraza la Mpito la Kusini (STC), linaloungwa mkono na Falme za Kiarabu (UAE).


Tukio hilo la kusikitisha limetokea Januari 2 (saa za huko), ambapo jumla ya wapiganaji 20 wa kundi hilo la wanaotaka kujitenga wameuawa papo hapo. Duru za usalama zinabainisha kuwa ndege za vita za Saudia zilidondosha 'mvua ya mabomu' katika kambi za kijeshi za Al-Kasha na Seiyun, hatua ambayo wachambuzi wa mambo ya kidiplomasia wanaitafsiri kama kugeuka kwa kibao katika vita vya muda mrefu nchini humo.


Msemaji wa STC amekaririwa na vyombo vya habari akieleza kuwa kambi ya Al-Kasha pekee ilishambuliwa mara saba mfululizo. Hii ni ishara kuwa Saudia imedhamiria kuwanyamazisha wapiganaji hawa ambao mwezi uliopita waliteka majimbo nyeti ya Hadramout na Al-Mahrah, yanayopakana na Saudi Arabia.


Kiini cha 'bifu' hili ni siasa na udhibiti. STC ni kundi linalopigania kurejeshwa kwa taifa la 'Yemen ya Kusini' ambalo lilikufa mwaka 1990 baada ya kuungana na Yemen ya Kaskazini. Wakati Saudia inaitambua na kuipigania Serikali Kuu ya Yemen inayotambuliwa kimataifa, washirika wao wa karibu, UAE, wamekuwa wakiwapa jeuri STC. Hii inafanya mgogoro huu kuwa na sura ya 'vita vya wakala' (proxy war) kati ya Saudia na UAE ndani ya ardhi ya Yemen.


Katika kile kinachoonekana kama kujibu mapigo kwa njia ya kidiplomasia na kisiasa, Mwenyekiti wa STC, Aidarus al-Zoubaidi, ameibuka kwenye runinga na kutangaza mpango mzito. "Ndani ya miaka miwili ijayo, tutaitisha kura ya maoni ili wananchi waamue hatima yao. Lengo letu ni kuwa na taifa huru litaloitwa 'South Arabia' (Arabia Kusini)," alitangaza Al-Zoubaidi kwa kujiamini.


Al-Zoubaidi hakuficha hisia zake, akionya jumuiya ya kimataifa kuwa endapo mazungumzo hayatofanyika au wakiendelea kushambuliwa kijeshi, hawatasita kutangaza uhuru huo "mara moja" bila hata kusubiri hiyo miaka miwili. Kauli hii ni kama kumwaga petroli kwenye moto, ikizingatiwa kuwa Saudia imetoa msimamo mkali kuwa haitaacha mashambulizi mpaka STC iondoke kwenye majimbo iliyoyateka.


Mgogoro huu unazidisha utata katika siasa za Mashariki ya Kati. Ikumbukwe kuwa STC na Serikali ya Yemen (inayoungwa mkono na Saudia) wote wana adui mmoja wa pamoja ambaye ni waasi wa Kihouthi (wanaoungwa mkono na Iran) walioko Kaskazini. Kitendo cha washirika hawa kuanza kupigana wenyewe kwa wenyewe kinatoa mwanya kwa Wahouthi kuimarika zaidi.


Wiki iliyopita, uhusiano kati ya Saudia na UAE ulifikia pabaya baada ya Saudia kushambulia meli iliyokuwa imebeba silaha kutoka UAE kwenda kwa STC. Ingawa UAE imetangaza kuanza kuondoa askari wake ili kupunguza joto, wachambuzi wanasema 'ngoma bado mbichi' na huenda Yemen ikaingia katika sura mpya ya umwagaji damu isipodhibitiwa haraka.

I recommend this article.

You can participate in article recommendations up to 50 times within 24 hours.


0 comments


Messages unrelated about this certain topic may be deleted or restricted.

0/300
Loading...

The copyright for this content belongs to the copyright holder or provider. Unauthorized use may result in legal liability under copyright laws and other regulations.