Mvutano mkali unaendelea kati ya Marekani na kundi la Wahouthi nchini Yemen, huku jeshi la Marekani likiripotiwa kufanya mashambulizi ya anga siku ya Jumapili, Aprili 13, 2025 (majira ya Yemen), karibu na mji mkuu, Sanaa. Mashambulizi hayo yalisababisha vifo vya watu wasiopungua sita na kuwajeruhi vibaya wengine kumi na tatu, kwa mujibu wa taarifa kutoka wizara ya afya inayosimamiwa na Wahouthi. Idadi hii ya wahanga iliongezeka kutoka ripoti za awali zilizotaja vifo viwili na majeruhi kumi.
Wizara hiyo pamoja na wakazi wa eneo hilo walieleza kuwa mashambulizi ya ndege za kivita za Marekani yalilenga kiwanda cha kutengeneza vigae (ceramics) kilichopo katika wilaya ya Bani Matar, viungani mwa Sanaa. Iliripotiwa kuwa sauti kubwa za ndege hizo zilisikika katika jiji zima la Sanaa kabla na baada ya mashambulizi hayo. Aidha, kituo cha televisheni cha Al-Masirah kinachoendeshwa na Wahouthi kiliripoti mashambulizi mengine ya ziada ya Marekani katika majimbo ya kaskazini ya Marib na Al-Jawf. Kwa ujumla, idadi ya mashambulizi ya anga yaliyofanywa na Marekani katika maeneo ya kaskazini mwa Yemen na Sanaa hivi karibuni inakadiriwa kufikia 25.
Mashambulizi haya ya Marekani yalifuatia tangazo la Wahouthi saa chache kabla, ambapo walidai kufanya mashambulizi dhidi ya maeneo matatu muhimu nchini Israeli. Maeneo hayo yalitjwa kuwa ni kambi ya kijeshi ya Sdot Micha iliyopo katikati mwa Israeli, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Ben Gurion, na "lengo muhimu" lingine ambalo halikutajwa jina katika eneo la Ashkelon, kusini mwa Israeli. Kwa upande wao, jeshi la Israeli lilikuwa limetangaza mapema kuwa lilifanikiwa kutungua kombora lililorushwa kutoka Yemen kabla ya kuingia katika anga la Israeli.
Hali ya wasiwasi na mapigano kati ya Wahouthi na majeshi ya Marekani imeongezeka tangu Marekani ilipoanzisha upya mashambulizi yake katika maeneo yanayodhibitiwa na Wahouthi tarehe 15 Machi. Serikali ya Marekani imesema kuwa mashambulizi yake yanalenga kuzuia uwezo wa Wahouthi kushambulia maeneo ya Israeli, ingawa hatua hizo zinaonekana kutofanikiwa kikamilifu kuzuia mashambulizi ya Wahouthi.
Kundi la Wahouthi, ambalo linadhibiti mji mkuu Sanaa na maeneo mengi ya kaskazini mwa Yemen, lilianza kushambulia meli zinazohusiana na Israeli katika Bahari ya Shamu tangu Novemba 2023. Wanasema hatua hizo ni sehemu ya kuwaunga mkono Wapalestina wanaokabiliwa na vita katika Ukanda wa Gaza. Wahouthi wameendelea kusisitiza kuwa watasitisha operesheni zao za kijeshi mara moja iwapo Israeli itakomesha mashambulizi yake dhidi ya Gaza na kuruhusu uingizwaji wa misaada ya dharura kama chakula na dawa bila vizuizi.
Katika kuonyesha msimamo wao mkali, Wahouthi walitoa taarifa tarehe 12 Aprili, wakionya kuwa jaribio lolote la Marekani kuanzisha operesheni ya ardhini nchini Yemen litasababisha matokeo mabaya ambayo yatafanana na "jehanamu". Onyo hilo lilitolewa kufuatia ripoti katika baadhi ya vyombo vya habari vya Yemen zilizodai kuwa Marekani inapanga kushirikiana na vikosi vya serikali ya Yemen inayotambulika kimataifa kufanya operesheni ya ardhini ili kuyakomboa maeneo yanayoshikiliwa na Wahouthi, ikiwemo Sanaa.
Chanzo cha picha: Xinhua