Hali ya usalama kwa jirani zetu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) imezidi kuwa tete na ya kutisha, ikithibitisha ule msemo wa wahenga kuwa "vita havina macho." Katika kipindi cha mwezi mmoja tu uliopita, kile kinachotajwa kama mauaji ya halaiki kimetokea Mashariki mwa nchi hiyo, ambapo zaidi ya raia 1,500 wamepoteza maisha kikatili kutokana na mashambulizi ya anga yanayotekelezwa na waasi wa M23.
Taarifa nzito iliyotolewa na Serikali ya Kinshasa na kunaswa na shirika la habari la AFP, imeanika ukatili huo unaofanywa kwa kutumia teknolojia ya kisasa ikiwemo ndege zisizo na rubani (drones) na mabomu mazito. Inasikitisha zaidi kubaini kuwa sehemu kubwa ya waliopoteza maisha katika mashambulizi hayo yaliyotokea mapema mwezi uliopita ni wanawake na watoto, makundi ambayo mara zote huwa wahanga wakuu 'tembo wanapopambana'.
Kidole cha lawama kimeendelea kuelekezwa kwa nchi jirani ya Rwanda. Licha ya kukanusha mara kwa mara, ripoti za wataalamu wa Umoja wa Mataifa (UN) zimezidi kugongelea msumari kuwa Rwanda ni "mfadhili mkuu" wa kundi la M23, ikidaiwa kupeleka takriban wanajeshi 4,000 kuwapa nguvu waasi hao ndani ya ardhi ya Kongo. Hii ni idadi kubwa ya askari wa kigeni inayochochea moto wa uhasama katika ukanda wa Maziwa Makuu.
Mpasuko huu mpya ulichochewa zaidi tarehe 5 ya mwezi uliopita, baada ya waasi wa M23 kufanya uvamizi wa kushtukiza katika jimbo la Kivu Kusini. Eneo hili ni nyeti sana kwani linapakana na nchi yetu ya Tanzania kupitia Ziwa Tanganyika. Kinachoumiza zaidi ni kwamba, uvamizi huu ulifanyika siku moja tu baada ya kile kilichotarajiwa kuwa 'mwanga wa matumaini'—mkataba wa amani uliofikiwa chini ya upatanishi wa Rais wa Marekani, Donald Trump. Tukio hili limetafsiriwa kama dharau ya wazi kwa juhudi za kidiplomasia za kimataifa.
Licha ya Marekani kuingilia kati tena na kushinikiza pande zote mbili (Jeshi la Kongo-FARDC na M23) kurudi nyuma umbali wa kilomita tano kutoka kwenye maeneo ya mapigano ili kuunda ukanda salama (buffer zone), hali bado ni ya "paka na panya." Mvutano bado ni mkali huku kila upande ukimtupia mwenzake lawama za kukiuka makubaliano. Kundi la M23, kwa upande wao, limekuja juu na kudai kuwa halihusiki na makubaliano hayo ya 'Trump' kwani hawakushirikishwa moja kwa moja mezani.
Kiini cha mgogoro huu, kama ilivyo ada kwa miongo kadhaa sasa, ni utajiri uliokithiri wa madini uliopo Mashariki mwa Kongo. Eneo hili limegeuka kuwa shamba la bibi ambapo zaidi ya vikundi 100 vya wanamgambo vinapigana vikugombea rasilimali hizo, huku wananchi wa kawaida wakiambulia mateso. Takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) zinatisha; zaidi ya watu milioni 7 wameyakimbia makazi yao, idadi ambayo ni kubwa kuliko wakazi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam. Hii ni janga la kibinadamu linalohitaji jicho la pekee kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na SADC.