Kanyewest Azuiwa Kuingia Australia Baada ya Wimbo Wenye Utata Kumtukuza Hitler

international | Thu Jul 03 2025


Kanyewest Azuiwa Kuingia Australia Baada ya Wimbo Wenye Utata Kumtukuza Hitler

Msanii maarufu wa muziki wa rap kutoka Marekani, Kanye West, maarufu kama Ye, amezuiwa kuingia nchini Australia kufuatia sintofahamu iliyozuka baada ya kuachia wimbo unaomtukuza Adolf Hitler. Uamuzi huu umethibitishwa na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Australia, Tony Burke.


Shirika la Habari la BBC lilimnukuu Waziri Burke akisema kuwa kibali cha West (visa) kilifutwa mapema mwezi Mei, muda mfupi baada ya wimbo wake uliokosolewa vikali, "Heil Hitler," kuwekwa wazi kwa umma. Haikubainika mara moja ikiwa kizuizi hiki cha kuingia nchini ni cha kudumu. Hata hivyo, Waziri Burke alifafanua kuwa "kwa mujibu wa sheria za Australia, kila maombi ya visa yanapitiwa upya."


Alipoulizwa kama hatua ya kufuta visa inaweza kuendelea, Waziri Burke alijibu kwa msisitizo kuwa "kuagiza chuki si jambo endelevu." Aliongeza, "Tayari tuna matatizo ya kutosha ndani ya nchi hii. Hakuna sababu ya kuagiza ubaguzi kwa makusudi." Kauli hii inaashiria uwezekano mkubwa kwamba kizuizi cha kuingia nchini kitaendelea kwa muda usiofahamika. Akiongea na kituo cha ABC cha Australia, Burke alisisitiza, "Ikiwa mtu yeyote atadai kuwa chuki dhidi ya Wayahudi ni jambo la busara, sitawaruhusu kuingia nchini hapa."


Wimbo "Heil Hitler," uliopo kwenye albamu mpya ya West, 'WW3', ulipata mamilioni ya watazamaji ndani ya saa 24 tu baada ya kutolewa mnamo Mei 8. Hata hivyo, wimbo huo umefutwa na kuzuiwa kwenye majukwaa makubwa ya kusikiliza muziki mtandaoni kama vile Spotify, Apple Music, na YouTube kutokana na maudhui yake yenye utata.


Mara baada ya wimbo huo kutolewa, West alidai kuwa "amewacha chuki dhidi ya Wayahudi" na kutoa toleo jipya la wimbo huo liitwalo "Hallelujah," ambalo lilifuta maneno yanayohusiana na Wanazi na kuyaweka maneno ya Kikristo.


Katika miaka ya hivi karibuni, Kanye West amekuwa chanzo cha mizozo inayoendelea kutokana na matamshi yake ya chuki dhidi ya Wayahudi. Mwanzoni mwa mwaka huu, alijitangaza kuwa Mnazi na pia alibatilisha ombi lake la msamaha alilowahi kutoa hapo awali. Kutokana na matamshi yake hayo, mnamo mwaka 2022, kampuni ya vifaa vya michezo ya Adidas ilitangaza kusitisha ushirikiano wake na West.

The copyright for this content belongs to the copyright holder or provider. Unauthorized use may result in legal liability under copyright laws and other regulations.