Mahusiano kati ya Azerbaijan na Urusi yameingia katika sintofahamu kubwa hivi karibuni, kufuatia hatua ya Azerbaijan kudai msamaha rasmi kutoka Urusi kuhusu tukio la ndege yao ya abiria kudunguliwa na kuanguka mwishoni mwa mwaka jana. Tukio hili linaongeza mkanganyiko katika uhusiano wa nchi hizo mbili ambao tayari ulikuwa na sura ya kutoelewana.
Rais wa Azerbaijan, Ilham Aliyev, alizungumza na waandishi wa habari mnamo Julai 19, akihoji ni kwanini Urusi haijachukua hatua stahiki kama nchi jirani inavyopaswa kufanya kufuatia ajali hiyo. Shirika la habari la Reuters limemnukuu Rais Aliyev akishutumu Urusi kwa kutochukua hatua zozote tangu tukio hilo la kudunguliwa kwa ndege. Rais Aliyev alisisitiza kuwa Azerbaijan inafahamu vyema kilichotokea na ina ushahidi wa kuthibitisha hilo. Aidha, alionyesha imani yake kuwa maafisa wa Urusi pia wanafahamu ukweli wa mambo.
Katika matakwa yake, Rais Aliyev alitaka Urusi ikubali rasmi kuhusika na tukio hilo, iwachukulie hatua za kisheria waliohusika, ilipe fidia kwa familia za waathirika na wale waliojeruhiwa, na pia ilipie gharama za ndege iliyoharibika. Alieleza kuwa matakwa haya ni "matarajio ya kawaida ndani ya mfumo wa sheria za kimataifa na mahusiano mema ya ujirani."
Ndege ya Azerbaijan Airlines, yenye namba ya usafiri J2 8243, iliyokuwa ikisafiri kutoka Baku, Azerbaijan kwenda Grozny, Urusi, ilianguka karibu na Aktau, magharibi mwa Kazakhstan, mnamo Desemba 25 mwaka jana. Katika ajali hiyo mbaya, watu 38 kati ya 67 waliokuwemo ndani ya ndege walipoteza maisha. Uchunguzi wa awali uliofanywa na mamlaka za Azerbaijan ulionyesha kuwa ndege hiyo ilipigwa na kombora la kupambana na ndege la Urusi au vipande vyake.
Licha ya Rais Vladimir Putin wa Urusi kumpigia simu Rais Aliyev Desemba 30 na kusema kuwa tukio hilo la kusikitisha lilitokea katika anga ya Urusi, hakutaja moja kwa moja kuwa Urusi ndio ilidungua ndege hiyo. Ikulu ya Kremlin pia haijawahi kukiri rasmi jukumu la Urusi katika ajali hiyo, ikisema tu kwamba mifumo yake ya ulinzi wa anga ilikuwa ikifukuza ndege zisizo na rubani (drones) za Ukraine wakati huo.
Kukosekana kwa msamaha rasmi kutoka Urusi kuhusu ajali ya ndege kumechangia kuzorota kwa mahusiano ya nchi hizo mbili mwaka huu. Hali ilizidi kuwa mbaya mwezi uliopita baada ya wanaume wawili raia wa Azerbaijan kufariki wakiwa kizuizini cha polisi huko Yekaterinburg, Urusi. Tukio hilo lilisababisha nchi zote mbili kuitana mabalozi wao, na hivyo kuongeza mivutano ya kidiplomasia.