Familia ya Daniel Chonchorio, mwanachama mkubwa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye inaripotiwa alipotea katika mazingira ya kutatanisha Jumapili asubuhi wakati akiwa kwenye mazoezi katika eneo la Nyakato jijini Mwanza, imeamua kujitokeza hadharani na kuomba msaada kutoka kwa wananchi wote.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Machi 25, 2025, dada wa mwanachama huyo, Lucy Mrimi, amesema familia yao imeingia katika hali ya sintofahamu kubwa na shughuli zote za familia zimesimama kutokana na kupotea kwa ndugu yao huyo katika mazingira ambayo hayajulikani.
Amesema mwanachama huyo, ambaye pia ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM Taifa, alitoweka Jumapili iliyopita, Machi 23, 2025, majira ya saa mbili asubuhi, alipokuwa anaelekea kwenye mazoezi kama kawaida. "Tunaamini vyombo vyetu vya usalama vinaweza kumtafuta na kumpata ndugu yetu na kuwakamata wahalifu waliohusika na ukatili huu. Tunawaomba Watanzania wote na hasa Rais wetu mpendwa, Samia Suluhu Hassan, atusaidie kwa hali na mali ili tuweze kumpata kaka yetu ambaye ni nguzo muhimu sana ya familia yetu," amesema Lucy kwa masikitiko.
Chonchorio, ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu na mkazi wa Nyakato jijini Mwanza, anadaiwa kupotea katika mazingira ya kutatanisha Jumapili asubuhi. Mbali na shughuli zake za biashara, hivi karibuni mwanachama huyo alitangaza nia yake ya kugombea ubunge katika Jimbo la Tarime Mjini kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
Jana, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, SACP Audax Majaliwa, alithibitisha kupokea taarifa za kupotea kwa mwanachama huyo na kueleza kuwa jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo la kusikitisha.